Visisitizi
Visisitizi hutumiwa kutilia mkazo nomino kwa kurejelea vionyeshi. Kwa mfano=
- Mtoto yuyu huyu
- Watoto wawa hawa
- Mpira uu huu
- Mipira ii hii.
Ni dhahiri kwamba kisisitizi cha kwanza huwa kimechukua silabi ya mwisho ya kionyeshi. Kwa sababu ya kanuni ya uchache wa silabi (neno la Kiswahili sharti liwe na silabi mbili au zaidi) irabu zote mbili za kionyeshi huweza kutumiwa kusisitiza nomino. Muundo wa visisitizi hutegemea ngeli ya nomino.
Kwa mfano:
NGELI | VISISITIZI |
LI | lili hili |
YA | yaya haya |
KI | kiki hiki |
A | yuyu huyu |
WA | wawa hawa |
U | uu huu |
I | ii hii |
VI | vivi hivi |
I | ii hii |
ZI | zizi hizi |
I | ii hii |
U | uu huu |
ZI | zizi hizi |
U | uu huu |
U | uu huu |
KU | kuku huku |
PA | papa hapa |
KU | kuku huku |
MU | mumu humu |
Mwanafunzi akizingatia kiambishingeli, anaweza kukisia usahihi wa visisitizi. Viambishi hivi vina ukuruba mwingi.
Vivumishi Vya Pekee
Vivumishi vya pekee ni maumbo -enye, -enyewe, -ote, -o-ote, na -ingine. Maumbo haya ndiyo tu huchanganya aina za viambishi vya upatanisho wa kisarufi vinavyojitokeza navyo kimatumizi.
Kwa mfano:
- mwanafunzi mwenye
- wanafunzi wenye
- mlingoti wenye
- milingoti yenye
- ukuta wenye
- kuta zenye.
Katika Kiswahili, hakuna maumbo mengine licha ya -enye na -enyewe yanayochanganya vivumishi vya upatanisho wa kisarufi. Hii ndiyo sababu ya kuyatambulisha maumbo haya kama ya pekee.
Umbo -ote huonyesha ujumla wa kitu au vitu. Kwa mfano:
- Watu wote wamefaulu.
- Kazi yote imekamilika.
Umbo -o-ote lina maana ya “kila”. Kwa mfano:
- Daktari yeyote atakutibu.
- Jumba lolote litanifaa.
Umbo -ingine huonyesha “tofauti na” au “zaidi ya”. Kwa mfano:
- Nchi zingine zina ubaguzi wa rangi.
- Wasichana wengine ni hodari kuliko wavulana.