MASHAIRI MEPESI

Shairi la Kwanza

Madawa ya Kulevya

1

Kwa fadha nasikitika, kuwaeleza bayana,

Machozi yananitoka, kufikiria vijana,

Ulevi wamejitwika, sio leo sio jana,

Kwa pamoja tuungane, tuyakatae madawa.

2

Kumi Kumi kumimina, wamefanya ni ibada,

Si wazee si vijana, wamefanza ndio ada,

Ya Muumba meyakana, meyakosea faida,

Kwa pamoja tuungane, tuyakatae madawa.

3

Madawa’yo kwa idadi, maradufu yamezidi,

Umma umeshashitadi, na kufanya ukaidi,

Ya ibura yamezidi, madawa yameshadidi,

Kwa pamoja tuungane, tuyakatae madawa.

4

Hashishi na kokenia, sio jambo la ajabu,

Ingawaje ni tanzia, na kitu kiso adibu,

Taabuni kujitia, madhila yametusibu,

Kwa pamoja tuungane, tuyakatae madawa.

5

Kilio kimetukumba, wanetu ‘meangamia,

Madawa yamewabeba, ‘mewaghururi dunia,

Staha mewaambaa, na hadhi kujishushia,

Kwa pamoja tuungane, tuyakatae madawa.

6

Kaditama nakingama, sendi mbele wala nyuma,

Yalo mema nimesema, sidhani mtalalama,

Namuombeni Karima, atuepushe salama,

Jamanini tuungane, tuyakatae madawa.

(Salim Swaleh, 2003)

Shairi la Pili

Sigara

1

Sigara kitu dhaifu

Madharake maradufu

Hukufanya uwe mfu

Hukupora utukufu

Kwenu, wachanga ni rafu

Hujitwika hu uchafu

Afadhali ule dafu

Ubaki mtu nadhifu

Kibwagizo:

Sigara sikupi nafasi

Nafsi yangu unajisi

Maisha yangu ni almasi

Kuipata si rahisi

2

Sigara ‘futa heshima

Huzidisha na gharama

Hushusha yako adhima

‘Kabaki bila karama

Maulana alalama

Watoto wape hekima

Ya kupinga wima wima

Huo moshi wa kuchoma

(Kibwagizo)

3

Sigara sawa laana

Sioni yake maana

Haina hata dhamana

Hufyeka yote hazina

Nawaita kwa mapana Vijana wote kungana Nia iwe kushikana

Masigara kuyakana (Kibwagizo)

4

Tamati Sigara duni Wavutaji ni Wahuni

Tabia zao ni ngeni Si wetu utamaduni

Tuikatie rufani

Sigara ‘siwe thamani

Uwe mwisho maishani

Isivume duniani.

(Kibwagizo)

(Abdul Fatahou, 2003)

Tags: 3306

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *